Search

Sermones

Somo la 9: Warumi (Maoni juu ya Kitabu cha Warumi)

[SURA YA 7-4] Miili Yetu Ambayo Inautumikia Mwili Tu (Warumi 7:14-25)

(Warumi 7:14-25)
“Kwa maana twajua ya kuwa torati asili yake ni ya rohoni; bali mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi. Maana sijui nifanyalo, kwa sababu lile nilipendalo, silitendi; bali lile nilichukialo ndilo ninalolitenda. Lakini kama nikilitenda lile nisilolipenda, naikiri ile sheria ya kuwa ni njema. Basi sasa si mimi nafsi yangu ninayetenda hilo, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu. Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa kutaka nataka, bali kutenda lililo jema sipati. Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Basi kama lile nisilolipenda ndilo nilitendalo si mimi nafsi yangu nilitendaye, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu. Basi nimeona sheria hii, ya kuwa kwangu mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya. Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu. Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.”
 

Jinsi Neema Yake Ilivyo ya Kushangaza!
 
Tunamtolea shukrani Mungu wetu ambaye ameturuhusu sisi katika kipindi hiki cha Mkutano wa Biblia wa Kiangazi na ambaye ameitawala hali ya hewa hali akizuia dhoruba na tufani na ambaye ametupatia sisi siku hizi njema. Mungu amezituma nafsi na amewakusanya watu wake pamoja ili aweze kutupatia Neno lake na kutufanya tufurahie katika ushirika kati yetu na pamoja na Roho Mtakatifu. 
Mungu yupo hai! Jinsi neema yake ilivyo ya kushangaza! Kwa sasa watu wanafikira kuwa kimbunga tufani kiitwacho “Doug” kwa hakika kitaipiga nchi yetu, hivyo maofisa wa serikali wamekuwa wakifanya doria ili kuwaondoa watu katika eneo la bonde la In-Jae. Leo mchana nilikwenda katika mji wa In-Jae. Niliwasikia watu wakizungumza hali wakiwa na hofu juu ya kimbunga hicho hali wakibuni jinsi kimbunga hicho kinavyoweza kuwa na nguvu kubwa na chenye uharibifu. 
Lakini je, kila kitu kitatokea katika namna ambayo wanaitarajia hata pale ambapo sisi watoto wa Mungu tumekusanyika hapa kwa ajili utulivu wa kiangazi? Ikiwa tutaomba, basi kwa hakika mvua haitanyesha kwa rehema za Mungu. Je, Mungu atawavurumishia mbali watu wake? Mungu anatawala juu ya hali ya hewa, lakini anafanya hivyo kutokana na imani yetu. Mungu anatenda kwa busara, na hii ina maanisha kuwa hataweza kuzijaribu imani zetu hasa sisi ambao imani zetu zimeanza tu hivi karibuni kwa kutufanya tushangae, “Kwa nini Mungu anatupatia kimbunga na tufani katika wakati huu ambapo tuna faragha ya kiangazi?” 
Mimi sikuwa na nguvu ya kuweza kukizuia kimbunga kiitwacho “Doug” mara niliposikia habari hizo. Kitu pekee ambacho niliweza kukifanya ilikuwa ni kuomba. Mkutano huu wa Biblia wa Kiangazi ulikuwa tayari umeshapangwa, tulikuwa tumeshakusanyika, na hakukuwa na kitu kingine ambacho tungeliweza kukifanya. Na nilikuwa na hofu kuwa kanisa hili linaweza lisiwe na nguvu ya kutosha kuweza kukihirimi kimbunga hicho hasa ukizingatia ule ukweli kuwa kanisa hili lilijengwa na vifaa ambavyo awali vilikuwa ni kama nguo. Hivyo sikuweza kufanya lolote zaidi ya kumtegemea Mungu. Niliomba, “Mungu utusaidie. Mungu utulinde. Ninaomba hivi katika Jina la Yesu Amin.” Na kwa kweli Mungu alikizuia kimbunga Doug! Ninaamini kuwa Mungu anafahamu kila kitu. Anatuongoza katika mahali salama kwa sababu anaifahamu hali yetu zaidi ya sisi tunavyofahamu. 
Hali ya hewa inatuonyesha kwa dakika kuwa Mungu yupo hai. Nilisikia kishindo cha ngurumo kama vile mlipuko wa bunduki katika hema langu. Basi nikatoka nje ya hema langu kisha nikaangalia angani. Anga lilikuwa ni jeusi na mawingu mazito yalikuwa yakitokea kila upande wa bonde lile. Hivyo nikaomba, “Bwana, je, mawingu yanakuja?” Imani yangu ikaanza kuwa dhaifu, “Mungu, nini kinaendelea? Je, kimbunga kimefika hapa? Je, ni kweli kuwa kimbunga kimefika hapa?” Lakini nilikuwa nimeomba na kuamini katika Mungu, na kisha nilikuwa nimeishikilia imani hii hali nikimwambia Mungu “Ninaamini kuwa Mungu utatutunza. Ninakuamini wewe. Nilikwisha amini kuwa Mungu utatenda kazi kwa ajili yetu.” Kwa kweli Mungu alitubariki kadri tulivyoomba. Tunamshukuru Mungu kwa mioyo yetu. 
 

Mwili ni Mbinafsi na Wenye Uovu
 
Sisi hatuwezi kufanya jambo lolote ikiwa Mungu hatendi kazi akiwa upande wetu. Mungu wetu anatutunza na anatusaidia. Hebu tuliangalie Neno la Mungu. Warumi 7:14-25 inatueleza sisi kuwa Mtume Paulo alijiona yeye mwenyewe kuwa anaishi katika mwili hali akiwa ameuzwa chini ya dhambi. Pia aligundua kuwa kwa sababu ya sheria mwili hauwezi kufanya lolote zaidi ya kuendelea kufanya dhambi muda wote atakapokuwa hai. 
Sisi ambao pia tumezaliwa tena upya tunatenda maovu, ingawa tunapenda kutenda mema kwa miili yetu. Warumi 7:19 inasema, “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” Tunafikia hatua ya kuona kuwa hakuna jema linalokaa ndani yetu. Kwa sababu ya jambo hilo tunashusha pumzi nzito kwa machungu hali tukiwaza, “je, ninaweza kuitunza na kuifuata imani yangu?” Tunatiwa uchungu sana kwa sababu ya kutokuwa na matumaini na mwili wetu wenye uovu. Je, unafahamu jinsi mwili ulivyo mbinafsi? Warumi 7:18 inasema, “Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa kutaka nataka, bali kutenda lililo jema sipati.”
Mara nyingi tunajichukulia upande wetu tu hata pale ambapo sisi ni mbegu ya watenda mabaya. Je, unafahamu jinsi tulivyo wabinafsi? Kwa hakika tunajifahamu kuwa sisi ni waovu, lakini hatujiweki katika upande wa Mungu bali tunasimama katika upande wetu tu. Kwa hakika Mungu ni mwema na mapenzi yake pia ni mema. Sisi tunajitambua kuwa tu waovu lakini bado tunajipenda wenyewe kupita kiasi. Mungu alituamuru sisi tusiwe na miungu mingine mbele zake. Mungu alitueleza hivi ili aweze kutupatia ufahamu kuhusu dhambi. 
Tunajipenda wenyewe na kufanya kila kitu kwa ajili yetu wenyewe hata pale tunapotambua jinsi tulivyo na ubinafsi na wenye kujitakia haki binafsi. Tunajisumbua pale kunapokuwa na kitu chenye faida kwetu, lakini tunanuka kiasi gani mbele za Bwana? Hii ni kwa sababu hatuna ufahamu. Watoto hawaruhusu biskuti zao kuondoka kirahisi. Wanashikilia kile kilicho katika mikono yao hadi kinapovunjika na hawapendi kushirikiana na mwingine kwa sababu wao bado ni watoto na hawana ufahamu wa kutosha. Hawafahamu kuwa kuna vitu vingine vya thamani katika ulimwengu huu zaidi ya bisikuti. Sisi tupo kama hao watoto. 
Dhambi zetu zilioshelewa mbali lakini ukweli ni kuwa sisi bado ni wabinafsi. Tunamshukuru Mungu kwa kutufanya sisi kuwa tusio na dhambi na kwa kutupatia Roho Mtakatifu kwa nguvu zake. Lakini vita inaanza ndani yetu wenyewe baada ya kuwa tumepokea ondoleo la dhambi na kuzaliwa tena upya. Vita hivi ni kati ya mwili na Roho. Mara baada ya kuzaliwa upya tunakuwa na furaha, lakini muda si mrefu tunaumizwa na vita hivi. Lakini Bwana anatuhitaji sisi ili tuweze kuifanya kazi kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. 
Bwana wetu aliuacha utukufu wake kwa ajili yetu. Alitumwa kuja katika mfano wa mwili. Hakutumwa kuja hapa ulimwenguni kama mtu mtanashati. Alikuja hapa ulimwenguni kama mtu mnyenyekevu. Kwa kweli, inasemekana kuwa Yesu hakuwa na utanashati wowote. Isaya alisema, “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, na kama mzizi katika nchi kavu; yeye hana umbo wala uzuri; na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani” (Isaya 53:2). Lakini, Bwana amezichukulia mbali dhambi zetu zote. 
Miili yetu inaitumikia dhambi tu. Paulo alifahamu kuwa mwili wake ulikuwa ni lundo la dhambi na hivyo akasema, “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo,” hata hivyo Mtume Paulo haelezei hili kwa kina kwa kuwa alikuwa akizionea aibu dhambi zake. 
Sisi ni kama mapipa ya takataka. Sisi ni lundo la dhambi. Tunaweza kukatishwa tamaa kiasi gani pale tutakapojiona tukiacha mnyororo wa taka nyuma yetu? Lakini hali tukiwa tumebanwa na dhamiri zetu tunajikuta tukimwambia Mungu, “Bwana, sipaswi kufanya hivi na ninapenda kuishi kwa kufuata mapenzi yako, lakini nimefanya tena kosa hili. Ninawezaje kuacha kutenda jambo hili Bwana?”
 

Tunaweza Kumshukuru Mungu Pale Tutakapoitambua Hali Yetu ya Uovu
 
Ni lazima tufikirie juu ya neema ambayo Yesu Kristo, Mungu wetu ametupatia. Ni lazima tufikirie kile ambacho Mungu alikifanya kwa mioyo yetu. Basi ni hapo tu ndipo tunapoweza kufahamu kile kilicho sahihi na ndipo tunapoweza kuanza kumtumikia Mungu. Ni kwa neema ya Mungu na imani yetu katika Mungu ndipo tunapoweza kumtafuta Mungu, kujitoa wenyewe kwake, na kisha kushinda changamoto yoyote ambayo inaweza kuwa inatusubiri kadri tunavyomfuata Mungu kwa mioyo yetu na kadri tunavyotembea pamoja naye. 
Mara nyingi tunaanza kujikana wenyewe tunapofikia kufahamu kuwa sisi ni waovu na tusio na maana mbele za Mungu. Tunatambua kuwa kuikwepa dhambi ni kitu kisichowezekana kwa sababu ya miili yetu, na kwamba hatuwezi kufanya lolote kwa sababu ya udhaifu wetu ingawa tumebarikiwa sana. Ninamtolea Mungu shukrani ambaye amenibariki ili niweze kumtumikia. Ikiwa Mungu angekuwa hajaniweka katika huduma ili kuitumikia injili, basi kwa hakika ningelikuwa nimebakia kuwa lundo la dhambi ambayo ilikuwa bado ipo katika mwili na nisingeweza kufanya kitu chochote cha haki mbele zake. 
Ninamshukuru Mungu kwa kuniwezesha mimi kumtumikia yeye. Hii ndiyo sababu ninatoa maombi kama haya. “Asante sana Bwana. Mungu ninahitaji fedha, lakini sina chochote. Ninapenda kufanya mambo haya yote kwa ajili yako ingawa sina kitu. Tafadhari naomba unisaidie. Sintazitumia fedha hizo kwa ajili yangu, bali kwa ajili ya Bwana. Ikiwa nitazitumia fedha hizo kwa ajili yangu, nina hakika mwili utakuwa na raha. Lakini ninapenda kuzitumia fedha hizo kwa ajili ya Bwana kwa ajili ya kazi ya haki. Fedha hizi ni za thamani kwangu, ninakutolea wewe. Naomba uzitumie kwa ajili ya kazi yako ya haki.”
Wale wanaoyafahamu maovu yao wanafahamu kuwa hakuna kitu chema kinachokaa ndani yao. Ninaposema “hakuna kitu chema kinachokaa ndani yao” nina maanisha nini? Ninamaanisha kuwa wao wana vitu viovu tu katika miili yao. Kwa kweli kuishi kwa ajili yako binafsi ni kitu kiovu. 
 

Tunamshukuru Mungu Kwa Kupitia Yesu Kristo Bwana Wetu 
 
Paulo alikiri kuwa, “Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi” (Warumi 7:24-25). Je, mwili unaitumikia nini? Kwa kweli mwili unaitumikia dhambi wakati wote. Hata hivyo, sisi tunamtumikia Mungu kwa mioyo yetu. Je, tunamshukuru Mungu kwa kupitia nani? Tunamshukuru Mungu kwa kupitia Yesu Kristo Bwana wetu. 
Paulo alisema, “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” Vivyo hivyo nami namshukuru Mungu. Ikiwa Bwana angekuwa hajazichulia mbali dhambi zangu zote, basi kwa hakika nisingeliweza kuokolewa kwa kuwa mwili bado unaitumikia dhambi hata sasa. 
“Namshukuru Mungu—kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” Tunamtolea Bwana shukrani kwa sababu alizichukulia mbali dhambi za miili yote. Hata baada ya kuwa tumepokea ondoleo la dhambi bado miili yetu inaitumikia dhambi tu. Lakini moyo unataka siku zote kumtumikia Mungu. Sababu inayotufanya tumshukuru Mungu na kwamba ni kwa nini moyo umefanywa kuwa wenye haki ni kwa sababu ya Yesu Kristo. Je, unaamini hivi? Tunamshukuru Mungu na tunamtumikia kwa sababu alizichukulia mbali dhambi zetu zote. Ikiwa Bwana angekuwa hajazichukulia mbali dhambi zetu na hajatuokoa toka katika dhambi za mwili, basi kwa hakika tungelikuwa tumeangamia milele. Je, unaamini hivi? 
Ikiwa Bwana angekuwa hajazichukulia mbali dhambi zetu tungeliwezaje kuwa na amani? Tungeliwezaje kumpatia Bwana shukrani? Na tungeliweza kumtumikia? Inawezekanaje kwa mtu aliye chini ya dhambi kuwasaidia watu wengine? Inawezekanaje kwa mtu aliye jela kuwakomboa wengine walio jela? “Namshukuru Mungu—kwa Yesu Kristo Bwana wetu” Bwana alizisafishia mbali dhambi zetu zote ili tuweze kumtumikia na ametupatia amani katika mioyo yetu. 
 

Sisi Tumekwisha Kufa Ulimwenguni
 
Tunawezaje kuihubiri injili, kumtumikia Mungu, kufanya kazi kwa ajili yake, na kisha kutoa mchango kwa huduma yake pasipo Bwana wetu? Sisi tunafanya haya mambo yote kwa kupitia Bwana wetu. Tunaendelea kumfuata Bwana leo, kesho, na kesho kutwa—hatubadiliki. Hii ndiyo imani sahihi. Wale wanaomtumikia Bwana ni kama wake wema na wenye busara wanaozitunza nyumba zao vizuri. Usiishi maisha mabaya ya kidini kama vile kikaango kinavyopoa haraka mara baada ya kuondolewa kwenye moto. Unapaswa kumfuata Bwana wakati wote mpaka pale atakapokuja tena. Hebu jichukulie mwenyewe kuwa umekatwa na kuondolewa toka katika ulimwengu baada ya kuzaliwa tena upya. Ninaomba ukumbuke kuwa wewe si mtu wa ulimwenguni tena. Sisi tumeishaufia ulimwengu. 
Majina yetu yameondolewa toka katika ukoo wa kifamilia wa ulimwenguni. Je, unafahamu? Majina yetu hayapo hapa duniani. 
Ulimwengu unaweza kukuambia, “Muda mrefu hatujaona chochote. Nini kinafuata? Nimesikia kuwa unahudhuria kanisani. Pia nimesikia kuwa dhambi zako zote zimesamehewa. Kwa hiyo hauna dhambi, eeh?” 
“Hapana, sina dhambi.” 
“Hilo ni jambo la kushangaza. Ninafikiri utakuwa umeangukia katika kanisa potofu.” 
“Hapana, usilitazame kanisa hilo kwa jinsi hiyo. Njoo kanisani kwangu. Utajionea mwenyewe jinsi lilivyo zuri.” 
“Bado ninafikiri kuwa unashida fulani.” 
Ndipo tunapofikiria, “Kwa nini hawanielewi? Ninatamani kama wangelinielewa.” Lakini, wale ambao bado hawajazaliwa tena upya wanaweza kutuelewa sisi? Inawezekanaje kwa watu ambao bado hawafahamu kuwa watu wanaweza kuwa wasio na dhambi wakatuelewa sisi? Wanawezaje kufahamu kuwa Yesu alizichukulia mbali dhambi zote za ulimwengu? Hawawezi kufahamu. Hivyo usitegemee kuwa watakuelewa. Bwana aliuambia ulimwengu kwaheri kwa ajili yetu. Alipunga kitambaa cha njano akiwa Msalabani. Bwana alisema, “imekwisha” (Yohana 19:30), wakati mwingine tunaweza kushindwa kuuambia ulimwengu kwaheri kwa sababu tunasukumwa na huruma. Pia Bwana alisema, “niliyaondoa majina yenu toka katika ukoo wa kifamilia wa ulimwengu.”
 

Bwana Alituwezesha Sisi Ambao Tusingeliweza Kumtumikia ili Tuweze Kumtumikia Kwa Kuzichukulia Mbali Dhambi Zetu Zote. 
 
Sisi, ambao tusingeliweza kumtumikia Bwana, tulifanywa kuwa wale tunaoweza kumtumikia Mungu kwa kupitia Yesu Kristo. Kwa asili, sisi tulikuwa ndio wale ambao tusingeliweza kumtumikia Bwana. Ni lazima tumsifu Bwana kwa kutuleta katika Kanisa lake na kutupitisha ili tuweze kumtumikia. Bwana anatutumia sisi. Kwa maneno mengine, Bwana anatutumia sisi katika kazi zake za haki. 
Wakati mmoja Mwinjilisti Lee alinukuu mfululizo wa mbolea katika mahubiri yake na akasema kuwa yeye alkuwa ni kama lundo la mboleo yenye kutoa harufu. Lakini hata hivyo bado alitumia maneno ya upole. Kusema kweli hali yetu ya dhambi haiwezi kulinganishwa na kitu chochote. Yeremia 17:9 inasema, “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote.” Mungu aliwawezesha wale ambao mioyo yao ilikuwa ni midanganyifu kuliko vitu vyote ili kuishi kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Mungu alituita ili tuweze kuifanya kazi yake ya haki. 
Tunaweza kumfuata Bwana na kuishi katika Neema yake kwa kuwa Bwana alizioshelea mbali dhambi zetu zote. Tunaweza kuteseka pamoja na Bwana na kisha tukatukuzwa pamoja naye. Sisi tulikwisha kufa kwa ajili ya Bwana. Ikiwa Bwana angelikuwa hajazichulia mbali dhambi zetu zote, basi kwa hakika tungekuwa tumeachwa nje ya wokovu. Kama tungeliendelea kuishi kwa kuufuata mwili basi tungekuwa tumebakia kuwa watu wa kidunia.
Bwana alituokoa sisi mara moja na kwa wakati wote milele. Alituokoa na kutufanya sisi kuwa vyombo vya huduma yake ya milele. Sisi ni wachafu na waovu kiasi gani? Baada ya kukutana na Bwana ndipo tunapofikia hatua ya kujitambua na kujiona jinsi tulivyokuwa wachafu na waovu. Hii ndiyo sababu tunafurahia sana mara tunapouona mwanga. Lakini tunapojiangalia sisi wenyewe, tunashusha pumzi kwa uzito kama Paulo alivyokiri, “Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?” (Warumi 7:24).
Lakini muda si mrefu Paulo alimsifu Bwana, “Namshukuru Mungu—kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” Bwana alizioshelea mbali dhambi zetu zote. Alizitoweshea mbali dhambi zote za mwili. Je, ni dhambi ngapi ambazo miili yetu inatenda kila siku? Usijifanye kana kwamba mwili wako hautendi dhambi. 
 

Je, Unamshukuru Bwana?
 
Bwana alizitoweshea mbali dhambi zote ambazo tunazifanya katika mwili. Je, unaamini? Kule kusema kuwa Bwana alizichukulia mbali dhambi zote za ulimwengu kunaweza kusionekane kuwa na umuhimu sana kwako, lakini ukitambua kuwa Bwana alizichukulia mbali dhambi zote zinazofanywa na mwili wako basi kwa hakika utapiga kelele ukisema, “Namshukuru Mungu—kwa Yesu Kristo Bwana wetu! Ninakusifu!”
Dhambi ina uzito wake. Bwana amezichukulia mbali dhambi zote tunazozifanya katika kipindi chote cha maisha yetu hadi siku ile ya mwisho. Je, hatupaswi kuwa na shukrani? Kama tungelifanya dhambi kidogo tungelimwomba Bwana msamaha kwa sala zetu za toba. Lakini dhambi ni nyingi zisizoisha na hazihesabiki hadi mwisho wa maisha yetu. Tunapotambua hivi, basi hatuwezi kufanya lolote zaidi ya kumsifu Mungu, “Asante sana Bwana. Umezitoweshea mbali dhambi zangu zote! Ninakusifu wewe!” Kwa maneno mengine, tunamshukuru Mungu “Kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” Je, unamshukuru Mungu na kukiri hivi? “Asante Bwana. Ninakushukuru kwa kuniita na kuniokoa ili niweze kuitumikia haki yako. Ninamshukuru Bwana aliyeniokoa toka katika dhambi zote za mwili.” Je, unamshukuru Bwana? Ukombozi wa kweli wa dhambi unaonekana kuwa ni rahisi kiasi hiki, lakini ukweli ni kuwa si kitu kinachopaswa kuchukuliwa kwa wepesi. Ni kitu kizito, kipana, kikubwa, cha thamani na cha milele. 
 

Ni lazima tumfuate Bwana Kwa Kuwa Hakuna Kitu cha Faida Ndani Yetu
 
Sisi ni lundo la dhambi. Ni lazima tufahamu kuwa sisi wenyewe ni kama giza tupu ndani yetu. “Mimi ni giza, bali wewe ni mwanga. Wewe ni mwanga wa kweli wakati mimi ni giza kamili. Wewe ni jua. Mimi ni mwezi.” Mwezi unaweza kuiangaza dunia pale tu inapokuwa imepata mwanga toka katika jua. 
Mwezi wenyewe hauwezi kutoa mwanga. Mwezi unaweza kutoa mwanga kwa kuakisi ule mwanga inaoupokea toka katika jua. Kila kitu ni giza. Je, wewe ni mwanga au ni giza? Pasipo Bwana sisi tupo katika giza. Sisi tunaweza kumshukuru, kumtumikia, na kisha kumfuata Mungu kwa sababu ya Yesu Kristo, kwa kuwa katika yeye hakuna hukumu ya adhabu. Kwa upande mwingine, kule kuitumikia miili yetu tu ni sawa na kulitumikia giza. Kama ni hivyo basi acha kufanya hivyo mapema kadri uwezavyo. Kwa kweli miili yetu haiwezi kubadilika hata tukijitahidi kiasi gani. Hakuna kitu cha upekee ndani yetu. Miili yetu haidumu milele na kwa hiyo tunapaswa kuishi kwa ajili ya vitu vitakavyodumu milele. Mtu yule anayeishi kwa ajili ya vitu vinavyodumu milele ni mtu mwenye busara. Ni lazima tujitambue mapema na kisha kuacha mabaya mapema. Ni lazima tufahamu kuwa hakuna kitu cha kutegemea toka kwetu na kwamba hakuna kitu kizuri ndani yetu. Sisi ni lundo la dhambi ambalo wakati wote linautumikia mwili. Mwili unasema, “Nipatie kitu chochote ninachokitaka,” na unafanya kama vile luba anayenyonya damu hali akiwa ameung’ang’ania mwili (Mithali 30:15). 
Baada ya kula kitu fulani tunajisikia njaa mara baada ya kwenda chooni. Miili yetu hairidhiki kamwe hata kama tukijitahidi kuitumikia kiasi gani. Mara nyingi tunajisikia njaa mara baada ya masaa machache bila kujalisha kiasi na ubora wa chakula tulichokula. Lakini ikiwa tunamshukuru Bwana na kumfuata yeye basi ni kweli kuwa furaha yetu inakuwa kubwa zaidi. 
Kwa kweli hatujisikii kuwa ni watupu pale tunapomfuata Bwana. Je, unapenda kuwa na furaha ya milele baada ya ukombozi wako? Basi ikiwa ni hivyo umfuate Bwana. Je, unapenda kuyaongoza maisha yako kuwa maisha ya nuru? Ikiwa ni hivyo basi umfuate Bwana. Je, unapenda kuishi maisha yenye neema? Ikiwa ni hivyo basi umfuate Bwana. Je, unapenda kuishi maisha yenye matunda tele? Basi utambue kuwa upo katika giza na kisha uifuate nuru. 
Sisi tunamfuata Bwana popote anapokwenda na tunasimama pale anaposimama. Sisi tunafanya kile ambacho Bwana anataka sisi tukifanye. Ni lazima tutembee pamoja naye na kisha tumfuate yeye. Je, una kitu chochote cha kukitegemea toka kwako wewe mwenyewe? Kwa kweli hapana! Ni lazima tumfuate Bwana kwa kuwa hakuna kitu cha kukitegemea toka kwetu. Je, mwili wako ni wa milele? Kwa kweli hapana! Basi ni kwa nini unakifuata kitu ambacho hakiwezi kukupatia chochote wala ambacho hakiwezi kudumu milele? 
Hapo zamani nilizoea kuimba wimbo unaosema hivi: “♪Nirudishie ujana wangu ♪” Lakini sasa nipo vizuri hata kama Mungu hataurudisha ujana wangu. Katika wazo la pili, nilitambua kuwa sintaweza kuwa na furaha ikiwa Mungu ataurudisha tena ujana wangu. Ikiwa tunamfuata Bwana ambaye ndiye nuru ya maisha yetu basi tufahamu kuwa taji ya utukufu imewekwa kwa ajili yetu. Hauhitajiki kurudi katika utoto wako tena. Badala yake sisi tunaimba, “♪Sintamkana Bwana na nitamfuata yeye kila siku katika siku zangu zote ♪” Hii inaonyesha imani ya kweli ambayo kwa hiyo hatuwezi kumkana Bwana katika maisha yetu na ambayo kwa hiyo tunamshukuru Mungu daima. Hebu tuuimbe wimbo huu wa injili!
“♪Ninampenda Mungu Bwana aliyemuumba mwanadamu toka katika mavumbi ya ardhi; ambaye alimpulizia mwanadamu pumzi ya uhai katika pua yake; ♫Na ambaye alimtuma Mwana wake kwa ajili yetu. Mimi nimeumbwa kwa mfano wake, kwa hiyo ninautoa mwili wangu kwa Bwana. ♫Sintamkana Bwana na nitamfuata yeye kila siku katika siku zangu zote. ♪”
 

Ninatoa Shukrani Halisi Kwa Bwana
 
Ninatoa shukrani halisi kwa Bwana. Bwana alizichukulia mbali dhambi zetu na alituwezesha sisi kumtumikia yeye, kumfuata, na kuifanya kazi yake ya haki. Sisi tungewezaje kuifanya kazi yake ya haki ikiwa Bwana angekuwa hajazitoweshea mbali dhambi zetu zote ambazo tunazifanya kila siku kwa miili yetu? Tusingeweza hata kama kwa asilimia 0.1%! Mwenye dhambi bado ni mwenye dhambi hata kama akiwa amelelewa vizuri kiasi gani. Ni jambo la kufurahisha kuona kuwa Bwana amezioshelea mbali dhambi zangu na kutuwezesha sisi kumtumikia. Ni jambo la kushangaza kuona kuwa Bwana ameziondolea mbali dhambi zetu zote na ametubariki sisi ambao tulikuwa tumezama katika uchafu katika maisha yetu yote, sisi ambao tulikuwa tukiishi kama wakosaji, tuliokuwa tumefungwa ili kwenda kuzimu, na tuliokuwa tukiishi maisha ya utupu pasipo kuwa na Bwana.
Kule kusema kuwa Bwana ametuchagua sisi ili kumtumikia yeye kwa kuzichukulia mbali dhambi zetu zote na kwa kutubariki kwa ukombozi wetu kwa imani kunaonyesha jinsi neema ya Mungu ilivyo kuu. Je, tunawezaje sisi kuwa wenye haki hali tukiwa na dhambi katika mioyo yetu? Ule ukweli kuwa sisi hatuna dhambi ni neema tosha na ya kipekee. Mungu asifiwe! Ukweli ni kuwa mwili utatenda dhambi tena. Hata kama tunalisikia Neno la Mungu sasa, ukweli ni kuwa tutatenda dhambi tena, na pengine mara baada ya kutoka ndani ya jengo hili la ibada. Kwa sababu ya hilo, ninamsifu Bwana kwa kuzioshelea mbali dhambi zetu zote. Bila shaka—Bwana wetu Yesu Kristo alizichukulia mbali dhambi zetu zote kwa ubatizo wake katika Mto Yordani na kisha akaimaliza hukumu ya dhambi juu ya Msalaba! Ninaamini na kumsifu Mungu! Sasa, tunawezaje basi kumsifu Mungu? Tunaweza kumsifu Mungu kwa kupitia Yesu Kristo!
Wapendwa watakatifu! Hatuwezi kutoa chochote kulipia neema ya Mungu hata kama tukijaribu kiasi gani katika maisha yetu yaliyosalia. Kwa kweli hata kama tukitoa shukrani kwa Bwana milele haitoshi, Bwana aliyetuwezesha sisi kuifanya kazi yake ya haki na kazi yenye matunda kwa kuzichukulia mbali dhambi zetu zote hata katika ule udhaifu tuliokuwa nao. Kwa kweli hata kama tutamsifu yeye katika siku zote za maisha yetu bado hatuwezi kumsifu vya kutosha. 
Kwa kweli tunafahamu kwa kina katika mawazo yetu kuwa hakuna kitu chema kilicho ndani yetu. Hebu fikiria tena jambo hilo. Je, utaendelea kutenda dhambi kadri unavyoishi? Kwa hakika utatenda dhambi, lakini Bwana amekwishazichukulia mbali dhambi zako. Bwana ametubariki kuifanya kazi ya Mungu. Bwana ametuwezesha sisi kumtumikia yeye. Hatuwezi kufanya lolote zaidi ya kumshukuru Bwana. Ninakusihi umsifu Bwana na kisha uishi maisha ya shukrani kwake kwa kupitia Yesu Kristo katika maisha yako yote. Mungu wetu ametuwezesha kuishi maisha ya shukrani kwa Mungu. Mungu ametuokoa toka katika dhambi zote tunazozifanya kwa mwili. Mungu ametuokoa toka katika dhambi zetu zote ili sisi tuweze kumtumikia yeye kwa mioyo yetu. Kwa kuwa neema ya Bwana wetu ni kubwa sana, basi sisi tunataka kumfuata na kumtumikia yeye. Hebu tumshukuru Bwana kwa mioyo yetu yote. 
Neema ya Mungu tuliyopewa kwa kupitia Yesu Kristo ni ya kushangaza sana! Kwa kweli ninapenda ufahamu jinsi mwili wako ulivyo mwovu na wenye udhaifu, katika hilo naomba ufikirie lile ambalo unalitenda, pia ufikirie ikiwa Bwana alizichukua mbali dhambi zako au la, umshukuru Bwana na kisha uishi kwa imani. Ninamshukuru Bwana aliyetuwezesha sisi kuishi maisha ya thamani. “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi” (Warumi 7:25). Sisi tunampenda Mungu kwa mioyo yetu lakini kwa miili yetu tunaipenda dhambi. Lakini Bwana wetu ni mwenye upendo zaidi. Dhambi haiwezi kuwa dhambi hadi tunapokuwa tumefanya tendo ambalo ni kinyume na maagizo ya Mungu kwa miili yetu, lakini hata hivyo Bwana wetu amekwishazitoweshea mbali dhambi zetu hata zile ambazo tutazitenda hapo baadaye. Hii ndiyo sababu kuwa Bwana wetu ni mwenye upendo zaidi na kwamba anastahili kushukuriwa. 
Asante sana Bwana. Ninakusifu kwa kutupatia mioyo ambayo kwa hiyo tunakutumikia na kwa kutuokoa kikamilifu toka katika dhambi zetu zote tulizozitenda katika kipindi chote cha maisha yetu.