Search

Maswali ya kila mara juu ya Imani ya Kikristo

Somo la 3: Ufunuo

3-6. Mji wa Yerusalemu Mpya ni Kitu gani?

Mji wa Yerusalemu Mpya ni Mji Mtakatifu katika Mbingu na Nchi Mpya ambayo Mungu amewaandalia watakatifu ambao watashiriki katika ufufuo wa kwanza. Baada ya kuyahitimisha mapigo ya mabakuli saba hapa duniani, Mungu atamfunga Shetani katika shimo la kuzimu lisilo na mwisho kwa miaka elfu moja, kisha atawapatia watakatifu walioshiriki katika ufufuo wa kwanza baraka ya kutawala milele pamoja na Bwana katika Ufalme wa Milenia, baada ya kuisha kwa miaka elfu moja, Mungu ataifanya mbingu na nchi ya kwanza kutoweka kisha atawapatia watakatifu zawadi ya Mbingu na Nchi Mpya. 
Wale ambao watazipokea baraka hizi ni watakatifu ambao wamepokea ondoleo la dhambi zao kwa kuamini katika injili takatifu ya maji na Roho iliyotolewa na Yesu Kristo. Bwana atafanyika kuwa Bwana-harusi wa watakatifu, na watakatifu watakuwa ni mabibi-harusi wa Mwana-kondoo ambaye amefanyika kuwa Bwana-harusi, watakatifu katika utukufu wakiwa wamevikwa ulinzi, baraka, na mamlaka ya Bwana-harusi katika Ufalme wake wenye utukufu. 
Mungu amewaandalia watakatifu hawa Mji Mtakatifu katika Mbingu na Nchi Mpya. Mji huu si mwingine bali ni Mji Mpya wa Yerusalemu. Mji huu umeandaliwa maalumu kwa watakatifu wa Mungu. Na mambo haya yote yamepangwa kwa watakatifu katika Yesu Kristo hata kabla Bwana Mungu hajauumba ulimwengu. Wale ambao kwa kuzitegemea nguvu za ajabu za Bwana Mungu, wataishi katika Ufalme wa Kristo wa Milenia basi hao wanastahilishwa kuingia katika Mbingu na Nchi Mpya ambapo Mji Mtakatifu unapatikana. 
Kuanzia wakati huu na kuendelea, watakatifu wataishi pamoja na Bwana milele katika Hekalu la Mungu. Kwa kuwa Mungu yupo pamoja nao, basi hakutakuwa na kifo tena, wala huzuni, wala kuomboleza, wala mateso, kwa kuwa mbingu na nchi ya kwanza vitakuwa vimepita, naye Mungu atafanya vitu vyote kuwa vipya. 
Mji wa Yerusalemu Mpya unang’ara, kwa kuwa una utukufu wa Mungu, na mwanga wake ni kama wa kito cha thamani, kama kito cha yakuti, kilicho angavu kama kioo. Hivyo, utukufu wa Mungu upo pamoja na mji na wale wote wanaoishi ndani yake. Mji una ukuta mkubwa na mrefu wenye milango kumi na mbili, milango mitatu kila upande; milango hii inalindwa na malaika kumi na mbili, na majina ya makabila kumi na mbili ya Israeli yameandikwa katika milango hiyo. Ukuta wa mji una misingi kumi na mbili, na juu yake yameandikwa majina ya mitume kumi na mbili wa Mwanakondo. 
Mji umewekwa kama mraba mkubwa, huku upande wake mmoja ukiwa na yadi 12,000—sawa na kilomita 2,220 (maili 1,390). Ukuta wake una dhiraa 144, ambazo ni takribani mita 72. Ukuta huu umejengwa kwa yakuti, na Mji ni wa dhahabu safi, kama vile kioo angavu. Misingi ya ukuta imepambwa kwa aina mbalimbali za vito vya thamani, na milango kumi na mbili ya mji imejengwa kwa lulu. 
Kwa kuwa Bwana Mungu na Mwana-kondoo wapo katika Mji, basi hakuna sababu ya mwanga wa jua wala mwezi. Pia mto wa maji ya uzima unatiririka toka katika kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-kondoo, huku ukiumwagilia Ufalme wa Mbinguni na kuvifanya vitu vyote kuwa vipya. Kila upande wa huo mto kuna mti wa uzima, unaozaa matunda kumi na mbili na kutoa matunda yake kila mwezi, na majani yake ni dawa ya kuwaponya mataifa. Katika mji huo hakuna tena laana, bali baraka za milele zinapatikana humo.