Search

Maswali ya kila mara juu ya Imani ya Kikristo

Somo la 3: Ufunuo

3-13. Mashahidi wawili wanafufuliwa na kunyakuliwa mbinguni baada ya kuukamilisha ushuhuda wao. Hii ina utofauti gani na kunyakuliwa kwa watakatifu kwa ujio wa Kristo mara ya pili?

Kama nilivyoeleza kwa majibu yangu kwa swali la 2, mashahidi hawa wawili ni watumishi maalumu wa Mungu ambao atawainua toka kwa watu wa Israeli ili kuwaokoa Waisraeli. Kuna kazi muhimu ambayo ni lazima Mungu ataifanya kabla ya kuuangamiza ulimwengu huu, na kazi hiyo ni kuwaokoa watu wa Israeli toka katika dhambi na kuwafanya washiriki katika ufufuo wa kwanza na unyakuo. 
Katika Warumi 3:29-30 Mtume Paulo anasema, “Au je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye Mungu wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia; kama kwa kweli Mungu ni mmoja, atakayewahesabia haki wale waliotahiriwa katika imani, nao wale wasiotahiriwa atawahesabia haki kwa njia ya imani iyo hiyo.” Njia ya kuokolewa toka katika dhambi mbele za Mungu ni sawa kwa Wayahudi na kwa Wamataifa pia. Kwa Wayahudi na kwa Wamataifa pia, wokovu unawajia kwa njia ya imani tu katika injili ya maji na Roho. Ili waweze kuokolewa toka katika dhambi zao zote, basi Wayahudi ni lazima wampokee Yesu Kristo kuwa ni Mwokozi wao na waweze kuamini, yaani kama Wamataifa walivyoamini, kwamba Yesu Kristo alizichukua dhambi zao zote katika mwili wake kwa ubatizo wake, na kwamba alikufa Msalabani ili kuhukumiwa kwa ajili ya dhambi kwa niaba yao. 
Mungu anawatendea Wayahudi pamoja na Wamataifa sawia, na amewaruhusu kupata wokovu kwa njia ya imani. Hii ndio sababu Mungu aliwaruhusu mashahidi wake wawili kwa watu wa Kiyahudi wakati wa miaka mitatu na nusu ya kwanza ya ile Dhiki Kuu, na ndio sababu Mungu aliwaruhusu mashahidi hawa kuihubiri injili ya maji na Roho kwao. 
Sura ya 11 ya Ufunuo inaelezea juu ya mizeituni miwili na vinara viwili vya taa ambavyo vinahusianishwa na mashahidi hawa wawili. Mizeituni miwili ina maanisha ni watumishi wawili wa Mungu ambao Mungu atawaruhusu kwa ajili ya wokovu wa Waisraeli, na vinara viwili vya taa vina maanisha ni makanisa mawili ya Mungu, ambayo ni kwa ajili ya Waisraeli na kwa ajili ya Wamataifa. Kwa maneno mengine, Mungu atayaruhusu Makanisa yake mawili kwa pamoja kuihubiri injili ya maji na Roho kwa Waisraeli na Wamataifa katika kipindi cha miaka mitatu na nusu ya kwanza katika ile miaka ya Dhiki Kuu. 
Hivi sasa, Kanisa la Mungu linapatikana kati ya Waisraeli. Lakini wakati Mungu anapoiangalia mioyo yao na wakati wake utakapowadia, Mungu ataiandaa mioyo yao kulipokea Neno lake, atawainua watumishi wawili kwa ajili yao, na atawafanya wampokee Yesu Kristo kuwa ni Mwokozi wao. 
Hivyo, Mungu atawaokoa Waisraeli na Wayahudi katika wakati wa Dhiki Kuu. Pia ataruhusu mateso na mauaji ya wafia-dini kwa watakatifu waliozaliwa tena upya kwa Waisraeli na kwa Wamataifa pia. Ule ukweli kwamba mashahidi wawili watauawa na kuwa wafia-dini baada ya kuutimiza ushuhuda wao na kisha kufufuliwa na kunyakuliwa mbinguni kwa siku tatu na nusu—basi, kama ilivyotokea kwa mashahidi hawa, vivyo hivyo watumishi wa Mungu na watu wake miongoni mwa Wamataifa watapambana dhidi ya Mpinga Kristo, watauawa na kuwa wafia-dini, na hivyo watashiriki katika ufufuo wao na katika unyakuo.