Search

Проповіді

Somo la 9: Warumi (Maoni juu ya Kitabu cha Warumi)

[SURA YA 8-12] Ni Nani Anayeweza Kudiriki Kusimama Kinyume Nasi? (Warumi 8:31-34)

(Warumi 8:31-34)
“Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” 
 

Katika Warumi 8:31-34, Paulo anashuhudia juu ya upendo wa Kristo usioweza kutenganishwa na waamini kwa kufanya majumlisho ya injili ya maji na Roho na kisha kufikia hitimisho lake la mwisho. Kifungu hiki kinaelezea furaha kuu ya wokovu ambayo imefikiwa katika kiwango cha juu cha imani. 
Katika Warumi 8:31, Paulo alisema, “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” Kama Paulo, sisi nasi tumepata uzoefu kwamba injili ya maji na Roho inang’ara zaidi kadri wakati unavyozidi kwenda na inazidi kuwa injili kubwa ya wokovu kadri udhaifu wetu unavyozidi kufunuliwa. Kadri tunavyozidi kuitumikia injili ya maji na Roho, basi ndivyo tunavyozidi kujazwa na uhakika na furaha. 
Paulo aliita ile injili ambayo aliiamini kuwa ni “injili yangu” (2 Timotheo 2:8). Injili ambayo Paulo anaishuhudia haikuwa nyingine zaidi ya imani katika ubatizo na damu ya Yesu. 
“Injili yangu” ambayo Paulo aliihubiri haimaanishi kuwa ni injili ya Msalaba ambayo watu wa kidunia wanaiamini, bali ni injili ya maji na Roho ambayo inaitangaza baraka kuwa Yesu alizichukulia mbali dhambi zote za mwanadamu mara moja na kwa wote. 
Injili hii ilimfanya Paulo kuwa ni mtu wa ujasiri sana. Kwa kuwa alikuwa ameupokea msamaha wa dhambi, basi haki ya Mungu iliujaza moyo wake na kwa sababu hiyo moyo wake ulijazwa na Roho Mtakatifu. Alijitoa katika kuubeba ushuhuda wa injili ya maji na Roho katika maisha yake yote. Injili ya maji na Roho ina nguvu na mamlaka ya kuzichukulia mbali dhambi za mwanadamu mara moja na kwa wote. 
Ni nani basi anayeweza kudiriki kuwa kinyume na injili ya maji na Roho ambayo Paulo aliiamini? Hakuna hata mmoja! Warumi 8:31 inatueleza kuwa, “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” Ni nani katika ulimwengu huu anayeweza kuwa kinyume na wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho? Wakati Mungu amemwokoa mwanadamu toka katika dhambi za ulimwengu kwa kupitia injili ya maji na Roho, ni nani anayeweza kuzichukua nguvu zake katika utupu? Si wale wanaomwamini Yesu kwa jina tu au wale wanaoamwamini Shetani wanaoweza kupingana na wanaoamini katika injili ya maji na Roho. 
 

Mungu Alituhesabia Haki Sisi Sote Mara Moja
 
Warumi 8:29-30 inasema, “Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki; hao akawatukuza.”
Hii inatueleza kuwa Mungu Baba alipanga kuwaokoa wenye dhambi wote katika Kristo na aliwaita kwa kupitia injili ya maji na Roho, akizioshelea mbali dhambi zao na kuwafanya kuwa watoto wake. Wakati Bwana wetu alipowakomboa wenye dhambi wote toka katika dhambi zao kwa kupitia injili ya maji na Roho, ni nani basi anayeweza kuwa kinyume na yale ambayo Mungu ameyafanya? 
Ni nani anayeweza kuwa kinyume na kuwashinda wale ambao wamehesabiwa haki kwa kuamini katika injili ya maji na Roho? Hakuna. Ni lazima utambue kuwa mtu yeyote ambaye yupo kinyume na wale ambao wamehesabiwa haki kwa kuamini katika injili ya maji na Roho basi mtu huyo yupo kinyume na Mungu mwenyewe. Ni lazima uamini katika injili ya maji na Roho na kisha uokolewe toka katika dhambi zako zote kwa gharama zote. Ikiwa katika akili zako na moyo wako upo kinyume na injili ya ukweli, basi hutaweza kuokolewa toka katika dhambi zako na utahukumiwa adhabu ya kwenda kuzimu. 
 

Hakuna Anayeweza Kuwa Kinyume na Wale Walio na Haki ya Mungu 
 
“Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” (Warumi 8:31). Kule kusema kuwa Mungu yupo upande wetu kunawasilisha ule ukweli kuwa Mungu amezichukulia mbali dhambi zetu zote kwa kupitia injili ya maji na Roho na ametuokoa. Ni nani basi anayeweza kuwa kinyume na wale waliokombolewa dhambi zao kwa kuamini katika injili ya maji na Roho, na ni nani anayeweza kusema kuwa imani hii ni potofu? Kwa kweli litakuwa ni zoezi la bure katika utupu. Mungu amezithibitisha imani za wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho. 
Inawezekanaje kwa mtu yeyote kuleta changamoto juu ya jambo hili? Yesu alizichukulia mbali dhambi zote za ulimwengu kwa kupitia ubatizo na damu yake Msalabani. Ni nani anayeweza kusema kuwa wale wanaoamini hivi wamekosea? Hakuna hata mmoja! 
Katika Warumi 6:3 Paulo alisema, “Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake?” Paulo alimaanisha kuwa yeye mwenyewe aliamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani, ambayo kwa hiyo dhambi zake zote zilipitishwa kwenda kwa Yesu na zikasafishwa, na ambapo Paulo alikufa na kufufuka pamoja na Yesu. 
Wagalatia 3:27 pia inatueleza kuwa, “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.” Kifungu hiki kinatueleza sisi kuwa Yesu alizichukua dhambi zote za ulimwengu katika mwili wake kwa ubatizo wake, na kwamba alisulubiwa Msalabani kwa ajili ya dhambi hizi, na kisha akafufuka ili kutupatia baraka ili kwamba wote wanaoamini katika ukweli huu wafanyike kuwa watoto wa Mungu. Imani ya Paulo ilijengwa katika imani kuwa alibatizwa katika Yesu, alikufa Msalabani pamoja na Yesu, na alifufuka pamoja naye. Kwa hiyo, mara unapoamini katika ubatizo wa Yesu, basi dhambi zako zote zinasafishwa na unafanyika kuwa mtoto wa Mungu kwa kufufuka pamoja na Kristo. 
“Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.” Kwa maneno mengine, wale wanaoamini kuwa Yesu alikuja hapa ulimwenguni na akabatizwa na Yohana Mbatizaji ili kuzichukua dhambi zote za ulimwengu katika mwili wake, watu hao wanabatizwa katika Yesu. Zaidi ya yote, watu hao pia wanaamini kuwa wamekufa Msalabani pamoja na Yesu na kwamba kwa imani yao wamefufuka pamoja naye. 
Kwahiyo yeyote anayeamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake ataokolewa toka katika dhambi zake. Kama ambavyo ni hakika kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, basi wote waliokombolewa dhambi zao kwa kuamini katika ubatizo na damu ya Kristo watafanyika kuwa watoto wa Mungu. “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.” Tunapoamini katika injili ya maji na Roho, basi tunaivaa haki ya Kristo ya kufanyika watoto wa Mungu. 
Paulo aliuzungumzia ubatizo wa Yesu kwa sababu aliipokea baraka kuu kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Lakini wengi bado hawajaipokea baraka ya jinsi hiyo toka kwa Mungu inayokuja kwa injili ya maji na Roho. Watu wengi wanafikiria kuwa injili ambayo Paulo aliihubiri ilikuwa ni injili ya damu ya Msalaba, lakini ukweli ni kuwa Paulo aliamini na kuitangaza injili ya maji na Roho ambayo inajumlisha ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani. 
Kwa nini basi wafuasi wa Yesu siku hizi hawaifahamu injili ya maji na Roho? Ni kwa sababu injili ya maji na Roho iliyohubiriwa katika kipindi cha Kanisa la Mwanzo imebadilika kadri wakati ulivyozidi kwenda. Katika kipindi cha Kanisa la Mwanzo, waamini wote waliamini na waliihubiri injili ya maji na Roho. 
Hata hivyo, kadri muda ulivyokwenda, injili hiyo ilianza kuhubiriwa kama ni injili ya damu ya Kristo tu wakati ubatizo wake ulizidi kuwekwa pembezoni. Hii ndio maana hata sasa kuna watu wengi ambao bado wanaamini juu ya damu ya Yesu tu Msalabani ambayo ni kinyume na ile injili iliyohubiriwa katika kipindi cha Kanisa la Mwanzo. 
Watu wanaoamini hivi bado wana dhambi katika mioyo yao. Hawaifahamu injili ya maji na Roho ambamo ndimo haki ya Mungu inamofunuliwa, na kwa sababu hiyo, wao wanabakia kuwa ni wenye dhambi na bado wapo kinyume na haki ya Mungu pamoja na kusema kuwa wanamwamini Yesu. 
Kipofu wa kiroho anaweza kuona nini? Kipofu anaweza kujaribu kumfahamu tembo alivyo kwa kumshikashika. Mtu asiyeona anaweza kugusa mguu wa tembo halafu akasema tembo yupo kama nguzo, na wakati huo huo kipofu mwingine anaweza kugusa pua ya tembo halafu akasema ni kama kitu kirefu kwa kuwa hajawahi kumwona tembo hapo kabla. Vivyo hivyo, mtu aliye kipofu wa kiroho hawezi kuzungumzia juu ya ukuu ya injili ya maji na Roho. 
Kwa hiyo, wale ambao hawaifahamu baraka ya maji na Roho hawawezi kuihuibiri. Wale wanaoweza kuona wanaweza kufahamu na kuelewa kile ambacho mtu anajaribu kukielezea kwa maneno, lakini kipofu hawezi kuelewa kitu hicho kwa kuwa hajakiona. 
Watu wanazaliwa wakiwa ni wenye dhambi. Kwa kuwa tulikuwa ni wenye dhambi kiroho tangu kuzaliwa kwetu, ndio maana hatuufahamu ukweli wa injili ya maji na Roho. Wale ambao wanaamini katika damu ya Msalaba tu wamejitengenezea toleo jingine la Ukristo wao wenyewe. Inawezekanaje kwa dhambi zao kuoshelewa mbali wakati wanadai kuwa wanamwamini Yesu katika damu ya Msalaba tu? Kitakachotokea hapo ni kuwa dhambi itazidi kulundikana zaidi kadri muda unavyozidi kwenda. 
Wale wanaoiamini damu ya Yesu tu kuwa ni wokovu wao ndio wale ambao hawajapata uamsho wa kiroho. Lakini Yesu anatueleza wazi katika Yohana 3:5, “Mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu.” Hivyo ni lazima tuamini katika injili ya maji na Roho ili tuweze kubarikiwa kwa utukufu wa kufanyika watoto wa Mungu na kisha kuingia katika Ufalme wa Mungu. 
Kwa kuwa Paulo aliamini katika injili ya maji na Roho, ndio maana basi alisema kwa imani, “Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?” (Warumi 8:31) Je, inawezekana kwa wale wasioifahamu injili ya maji na Roho wakawa kinyume na watoto wa Mungu? Wanaweza kuwa kinyume na watoto wa Mungu, lakini hawawezi kuwashinda kamwe. Wale ambao wanaiamini damu ya Msalaba tu hawawezi kuwashinda wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho. 
Wale walio kinyume na haki ya Mungu wanaweza kufanyika maadui wa Mungu na kwa hiyo hawawezi kuzipokea baraka zake. Hakuna anayeweza kupokea wokovu au kuwa na imani ambayo inampeleka mbinguni pasipo kuiamini injili ya maji na Roho, injili ambayo haki ya Mungu inafunuliwa. Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wanaweza basi kuishinda injili ya uongo na kisha kuirudia injili ya kweli. Watoto wa Mungu wanaweza kuushinda ulimwengu na Ibilisi mwenyewe. 
Baadhi hawaufahamu vizuri ubatizo wa Yesu na damu yake, na kule kutofahamu kwao kunawaongoza kwenda katika imani potofu. Ikiwa unaamini katika damu ya Yesu halafu haufikirii sana juu ya kupokea msamaha wa dhambi kwa kuamini katika injili ya ubatizo wa Yesu basi imani yako ni potofu. 
Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho ndio wale ambao wataipata haki ya Mungu na kuwa na imani ya kweli mbele za Mungu. Mungu anatueleza sisi kuwa wale wanaoamini katika damu ya Mwana wake Msalabani tu wamekosea. Wale wasio iamini haki yake ndio hao ambao hawaiamini injili ya maji na Roho, lakini wale wanaoiamini haki yake ndio hao wanaoamini katika damu ya Yesu Msalabani na ubatizo wa Yesu kuwa ndivyo vilivyozichukulia mbali dhambi zao. 
Ni lazima tuachilie mbali ugumu wetu wa mioyo. Wale ambao wanaikataa injili ya maji na Roho wanakazia kuwa imani zao potofu ndizo za kweli. Wale ambao wanaamini juu ya damu ya Yesu Msalabani tu wana imani iliyo nusu katika haki ya Mungu. Ni wale tu wanaoamini katika injili ya maji na Roho ndio walio na imani yote kamilifu, na ni hao peke yao wanaoamini katika haki ya Mungu na kuipata (Mathayo 3:15, 11:11).
Vitabu vilivyoandikwa na wale ambao wanaamini juu ya damu ya Yesu tu kwa kweli wanaharibu karatasi. Yale mafundisho ya kidini ambayo yaliwahi kujadiliwa na watheolojia hivi sasa yanadharauliwa na Wakristo, lakini injili ya maji na Roho inakubaliwa sana hivi sasa. Ukweli huu umekuwepo tangu kipindi cha Mitume na hautabadilika. Neno la Mungu linadumu milele, lakini wale wanaoamini katika damu ya Yesu tu wataondolewa toka katika kumbukumbu za watu. Kwa sababu gani? Ni kwa sababu damu, ambayo ina nusu ya haki ya Mungu, haina lolote la kufanya kuhusiana na mwenye dhambi mwenyewe. 
Nikisema wazi, watu wengi siku hizi bila kujali kuwa ni Wakristo au si Wakristo, wanafanya dhambi nyingi sana. Inawezekanaje basi kwa dhambi hizi zote kusamehewa kwa kuamini katika damu peke yake? Mafundisho ya kidini ambayo yanasisitiza juu ya damu ya Msalaba tu yanawafundisha watu kuomba sala za toba kila wanapofanya dhambi, lakini wataendelea kuomba hiyo toba kwa muda gani? Hata wakisema au kuomba vipi watu hao hawawezi kupokea msamaha wa dhambi. 
Je, Yesu alikuja hapa ulimwenguni halafu akamwaga damu yake Msabalani bila kubatizwa? Unafahamu kuwa huu si ukweli. Yesu alikuja hapa ulimwengu akazichukua dhambi zote kwa kubatizwa (Mathayo 3:15). Yesu alibatizwa na Yohana kabla ya kuimwaga damu yake Msalabani, na hivyo ubatizo ule ukamruhusu kusulubiwa Msalabani. Hivi ndivyo Yesu alivyoitimiza haki yote. Ikiwa unaamini juu ya ubatizo ambao Yesu aliupokea toka kwa Yohana, basi huna haja ya kuendelea kulia kwa ajili kuipata rehema ya kusamehewa dhambi kila siku. Badala yake, amini katika haki ya Mungu na kisha upokee wokovu mkamilifu. 
Yesu alibatizwa ili kuzichukua dhambi zote za ulimwengu katika mwili wake na alisulubiwa ili kuhukumiwa adhabu kwa ajili ya dhambi hizo za ulimwengu mara moja na kwa ajili ya wote. Ukombozi unaweza kupatikana kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake. 
 

Je, Yesu Alitupatia Wokovu Ambao ni Mkuu Kuliko Dhambi Tunazozitenda? 
 
Ukombozi uliotolewa na Yesu ni mkubwa sana kuliko dhambi zote tunazozifanya na ambazo tutazifanya. Ikiwa ubatizo wa Yesu na damu yake visingekuwa na ukuu kuliko dhambi za wanadamu, basi tusingeweza kumwamini Yesu kuwa ni Mwokozi na wala tusingeweza kuupata ukombozi. Hata hivyo, uzuri wa Bwana ni mkubwa sana kiasi kuwa alizichukulia mbali dhambi za ulimwengu mara moja na kwa ajili ya wote kwa kupitia ubatizo wake. 
Vivyo hivyo, lango la Mbinguni liko wazi, lakini hakuna anayeweza kuingia katika lango hili pasipo kuamini katika injili ya maji na Roho. Unaweza kuwa kinyume na wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho, lakini ukweli ni kuwa hutaweza kujificha na kuikwepa hukumu ya Mungu ya kutisha. Kwa hiyo, usifikiri kuwa unaweza kuishinda imani katika ubatizo na damu ya Yesu ambayo kwa hiyo haki ya Mungu imetimizwa. 
Wale wote waliokuwa kinyume na injili ya maji na Roho pia walikuwa kinyume na Mtume paulo. Lakini hakuna hata mmoja aliyedirikia kusema kuwa injili ya maji na Roho ambayo ilihubiriwa na kuaminiwa na Paulo kuwa ilikuwa na makosa. Wao waliweza kukiri kuwa Yesu alikuwa ni Mwana wa Mungu na Mwokozi wao. 
Warumi 8:32 inatueleza kuwa, “Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia mambo yote pamoja naye?” Mungu Baba alimtuma Mwanawe pekee hapa ulimwenguni na akamfanya kubeba dhambi zote za ulimwengu kwa kupitia ubatizo wake, kufa Msalabani, na kufufuka tena toka kwa wafu ili kutukomboa toka katika dhambi zetu. 
Mungu Baba alitupatia sisi Mwanawe pekee ili kutuokoa toka katika dhambi za ulimwengu na kutufanya sisi kuwa watoto wake kama Yesu alivyokuwa. Mungu alimtuma Mwanawe pekee kubatizwa ili aweze kuwafanya wote wanaoamini katika injili ya maji na Roho kuwa watoto wake, wenye haki na waliobarikiwa. Mungu alikuwa amepanga kumpatia mwanadamu baraka zote za mbinguni na injili ya maji na Roho. Moja kati ya baraka hizi ni kufanyika watoto wake kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. 
“Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia mambo yote pamoja naye?” (Warumi 8:32). Neno “Mambo yote” lina maanisha kuwa ni karama za Mungu. Karama zipi? Mungu aliwapatia haki ya kufanyika watoto wa Mungu wale wote waliompokea Yesu na kumwamini—yaani wale walioiamini injili ya maji na Roho walifanywa na wanafanywa kuwa watoto wa Mungu. Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho hawana dhambi. Wao ni wenye haki na ni watoto wa Mungu waliotakaswa kwa kweli. 
Wale wanaofanyika kuwa watoto wa Mungu kwa kuamini katika haya yote watapewa zawadi ya Ufalme wa Miaka Elfu Moja na Ufalme wa Mbinguni. Wenye haki wamebarikiwa ili kurithi utukufu wote wa Mbinguni. 
“Kutukirimia Mambo haya yote” kauli hii imetafsiriwa na baadhi kuwa ni kule kukirimiwa Roho Mtakatifu. Wao wanafikiria kuwa, “Je, hii ina maanisha kuwa mara tunaomwamini Yesu, tutapewa Roho Mtakatifu kipekee?” Hii si kweli kwa sababu unapoamini katika injili ya maji na Roho, unapokea ondoleo la dhambi zako na Roho Mtakatifu kwa wakati mmoja. Roho Mtakatifu hawezi kukaa katika moyo wenye dhambi. Roho Mtakatifu anakuja kwetu kila wakati dhambi zetu zinapokuwa zimesamehewa. 
Kuna zaidi kwa waamini kuliko kupokea Roho Mtakatifu. Karama za Mungu haziishi hadi baraka zote za mbinguni zinapokuwa zimetolewa kwetu. Katika ulimwengu huu, watu wanafikiri kuwa ule uwezo kama vile kuponya, kunena kwa lugha, na kutabiri ni karama, lakini karama inayotajwa katika kifungu hiki inazungumzia juu ya mambo yote ya mbinguni ambayo Baba yetu anayamiliki. Paulo anapoongolea juu ya karama anazungumzia juu ya mambo yote ambayo Mungu anawapatia watoto wake walio na haki ya Mungu. 
Mungu alisema kuwa atawapatia mambo mema yote kama karama kwa wale wote wanaoamini katika injili ya maji na Roho. Mungu aliitoa karama ya kuzaliwa tena upya kwa wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho. Mungu anatoa mambo yote Mbinguni kama zawadi kwa wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho. Wakristo wanateseka sana wapokuwa wakiishi katika ulimwengu huu lakini Ufalme wa Mungu utakapokuja watavikwa utukufu wa Mbinguni. 
 

Usiseme Kuwa Wewe ni Mteule Pasipo Sababu 
 
Warumi 8:33-34 states, “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki, Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.”
“Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu?” Je, unaweza kuwashtaki wale ambao Mungu amewaokoa kwa injili ya maji na Roho? Kwa kweli hapana! 
Watheolojia wanamnukuu Kalvin wakisema kuwa baadhi ya watu waliteuliwa pasipo sababu hali wengine waliachwa. Hata hivyo, hatupaswi kutumia neno “pasipo sababu” mbele ya uwepo wa Mungu. Maana kwa kufanya hivyo wanathibitisha kuwa hawamfahamu Mungu kabisa, na kwamba fundisho lao la dini ni la uongo. Kuteuliwa au kuchaguliwa pasipo sababu maana yake ni kuwa Mungu anawapenda baadhi bila sababu yoyote na anawachukia wengine pasipo sababu yoyote pia. Tunawezaje kusema kuwa Mungu ni mwenye haki wakati anawapenda wengine na kuwachukia wengine? Kwa kweli huyu si Mungu wetu. Mungu wetu anawapenda na kuwajali wanadamu wote katika Kristo. 
Hapa katika aya ya 32 panasomeka hivi, “Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia mambo yote pamoja naye?” Mungu alitupatia Mwana wake ili kuwaokoa wanadamu wote. Kwa kupitia Mwana wake, Mungu alitufanya sisi kuamini kuwa Yesu amezichukulia mbali dhambi zetu zote kwa kupitia Neno la maji na damu. Katika aya ya 33 imeandikwa hivi, “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu?” Neno “wateule wa Mungu” halimaanisha kuwa Mungu anawachagua baadhi ya watu bila sababu. Mungu anawachagua wote wanaoishi pasipo kuwa na Yesu Kristo na wale wasio na haki yao binafsi ili aweze kuwavika haki yake. 
Wale waliochaguliwa na haki ya Mungu ni wale ambao wanaamini na kukaa katika ukweli kuwa Yesu alikuja hapa duniani, alibatizwa, alisulubiwa Msalabani ili kuziondolea mbali dhambi zetu zote. Hao ndio wale wanaomwamini Mungu ambaye amewaokoa toka katika dhambi za ulimwengu na aliyewavika kwa haki yake. 
Ni nani basi anaweza kuwashtaki wenye haki? Hakuna! Hakuna anayeweza kusema kuwa imani yetu ni potofu. Hakuna anayeweza kuwahukumia adhabu wale waliookolewa toka katika dhambi zao na ambao wamefanyika kuwa watoto wa Mungu kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Wale wanaoamini katika damu ya Msalaba tu pia hawawezi kusema kuwa wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wana makosa, wala hawawezi kuleta mashtaka dhidi yao mbele za Mungu. 
Baadhi ya watu wanawahukumu kimakosa wale ambao wamefunikwa na haki ya Mungu kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Lakini hiyo ni sahihi? Hapana! Imani ya wale waliochaguliwa kuwa wenye haki katika uwepo wa Mungu haiwezi kuhumikiwa kimakosa na mtu yeyote. 
Ni nani anayeweza kusema kuwa wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho ni wenye dhambi na wakaihukumu imani yao kimakosa? Tumekuwa tukihubiri injili ya maji na Roho, injili ambayo haki ya Mungu imedhihirishwa kwa muda mrefu kwa watu wote ulimwenguni. 
Lakini hakuna hata mmoja aliyetuletea mashtaka kwa kuihubiri injili ya maji na Roho. Kulikuwa na wachache waliotuomba kuithibitisha imani katika damu ya Msalaba tu. Hata wao hawakuweza kusema kuwa kuwa na imani katika injili ya maji na Roho ni kosa. 
Injili ya kweli ya maji na Roho ni injili iliyo na haki ya Mungu. Hii ni injili ya kweli na injili nyingine zote nje ya hii si injili kamilifu. Mtume Paulo, ambaye aliihubiri injili ya maji na Roho alisema kuwa hakuna injili nyingine zaidi ya injili hii ya kweli na akatamka kuwa, “Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yoyote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe. Kama tulivyotangulia kusema, na sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yoyote isipokuwa hiyo mliyoipokea na alaaniwe” (Wagalatia 1:8-9).
Hakuna anayeweza kusema kuwa injili ya maji na Roho ina makosa kibiblia. Wale wasio amini katika injili ya maji na Roho wapo kinyume na Biblia. Ikiwa unaamini kuwa injili ya maji na Roho iliyotolewa na Mungu ni potofu, basi endelea kupingana na Mungu. Sisi pia tunaweza kupingana na injili zisizo kamili na zenye makosa, yaani injili ambazo zinakazia juu ya damu ya Yesu tu Msalabani. Inawezekanaje kwa Yesu kusulubiwa kwa ajili ya dhambi zetu pasipo kwanza kuzichukua katika mwili wake kwa ubatizo wake? 
 

Usiseme Kuwa Waamini wa Haki ya Mungu Wana Dhambi 
 
“Kuwashtaki” maana yake ni kuomba hukumu katika kesi. Mtu pekee anayeweza kuleta mashtaka juu ya wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho ni yule mtenda maovu. Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wana imani katika haki ya Mungu, na kama hivyo ni nani basi anayeweza kuihukumu vibaya imani yao? Ni nani anayeweza kusema kuwa wana makosa? Hakuna hata mmoja, kwa kuwa ni Mungu ndiye anayewahesabia haki. Hakuna anayeweza kuwashutumu waamini wa injili ya maji na Roho kuwa wana dhambi. 
“Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki” (Warumi 8:33). Ni nani anayeweza kutangaza kuwa waamini wa injili ya maji na Roho hawana dhambi? Ni Mungu ndiye anayeweza. Mungu anatangaza kwa haki yake kuwa waamini wa injili ya maji na Roho wamehesabiwa haki. 
“Kuhesabiwa haki” hakuwahusu wale ambao bado wana dhambi, bali kunawahusu wale ambao dhambi zao zilisamehewa, wakafanywa kuwa “wasio na dhambi na waliohesabiwa haki.” Wakati Mungu anasema kuwa wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho si wenye dhambi, ni nani basi anayeweza kudiriki kusema kuwa wana makosa na hawana haki ya Mungu? Hakuna mwanatheolojia katika ulimwengu huu anayeweza kusema hivyo. 
Ukristo wa leo umeharibiwa na Fundisho la Utakaso ambalo linajaribu kuupata utakatifu wa kidini. Mwanatheolojia mmoja huko Uingereza aliulizwa hivi, “Je, Kanisa la Mungu ni takatifu?,” yeye alidai kuwa kanisa la Mungu pia lina makosa na uchafu. Ni wazi kuwa mwanatheolojia huyu alikuwa haifahamu injili ya maji na Roho na wala hakuwa na imani katika haki ya Mungu. 
Lakini kila mwamini katika kanisa la Mungu anayeamini katika injili ya maji na Roho hana dhambi kabisa. Ingawa mwamini huyo anaweza kuwa dhaifu katika mwili, ukweli ni kuwa mtu huyo bado ana ile haki ya Mungu iliyo safi na kamilifu. 
Je, kila mtu katika kanisa la Mungu hana dhambi? Ndiyo! Kanisa ni mahali ambapo waamini ambao wametakaswa na wasio na dhambi wanakutana pamoja katika Kristo. Ikiwa waamini wana dhambi basi wao si watoto wa Mungu. Ni kitu gani kilichowafanya watakaswe? Kwa kweli ni imani katika injili ya maji na Roho ambayo imewafanya wao kuwa wasio na dhambi kwa kuipokea haki ya Mungu. Mtheolojia alisema kuwa hata kanisa la Mungu lina dhambi kwa kuwa alikuwa haamini wala haifahamu injili ya maji na Roho. 
Ni nani anayeweza kudiriki kusema kuwa waamini wa injili ya maji na Roho ni wenye dhambi? Ni Mungu ndiye mwenye “kuwahesabia haki”. Je, sisi tunaoamini katika injili ya maji na Roho tunaweza kuwa na dhambi ati kwa kuwa sisi ni wadhaifu? Kwa kweli hatuwezi! Je, hii ina maanisha kuwa hatuna dhambi hata pale ambapo bado tunatenda dhambi? Ndiyo, hatuna dhambi! Hii ndiyo sababu tunahitaji kuiamini injili ya maji na Roho. Watu hawapendi kutenda dhambi kwa makusudi bali ni kwa sababu ya udhaifu wao. 
Kuna watu wachache sana ambao kwa kweli wanadhamiria kutenda dhambi; lakini karibu sehemu kubwa ya maovu ya mwanadamu inasababishwa na udhaifu wa wanadamu. Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho hawana dhambi katika mioyo yao kwa sababu wana haki ya Mungu. Sisi hatuna dhambi kwa sababu Mungu alikwisha shughulikia masuala ya dhambi zetu zote kwa haki yake. Ndio maana Biblia inasema, “Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki.” Ni Mungu ndiye anayetangaza kuwa waamini wa injili ya maji na Roho hawana dhambi kwa kuwa wana haki yake. Tumekombolewa toka katika dhambi zetu zote kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. 
Ikiwa Yesu angekuwa hajazichukua hata zile dhambi zetu zinazokuja, tungeliwezaje basi kukombolewa dhambi zetu na tungeliwezaje kusema kuwa sisi si wenye dhambi kabisa? Ikiwa baada ya kuiamini haki ya Mungu tunatenda dhambi na kuishi katika dhambi, je, hii ina maanisha kuwa hatujatakaswa vizuri, au je, hali hiyo inaondoa sifa ya ukombozi wetu na kuturudisha tena kuzimu? Jibu ni hapana! Ikiwa wokovu wetu unakuja kwa kutakaswa binafsi, ni nani basi katika ulimwengu huu ambaye angeliokolewa? Hakuna hata mmoja! Hakuna anayeweza kuishi maisha makamilifu katika mwili na kutakaswa kwa kuzitunza na kuzishika amri zote kikamilifu. Ndio maana Biblia inasema, “Hakuna mwenye haki hata mmoja” (Warumi 3:10).
 

Kwa Asili, Wanadamu Hawawezi Kuipokea Haki ya Mungu Kwa Matendo Yao Wenyewe
 
Mungu alimtuma Mwanawe pekee ambaye alibatizwa na Yohana Mbatizaji, kisha akamfanya auawe Msalabani ili kuwaokoa wanadamu wote toka katika dhambi za ulimwengu. Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wamefanyika kuwa wenye haki kwa imani. Hii ndiyo sababu kunaweza kuwa na wenye haki hata katika ulimwengu huu. Ibrahimu pia alifanyika kuwa baba wa imani kwa kuliamini Neno la Mungu. 
Ingawa Wakristo wengi wanasema kuwa wanaweza kupokea haki ya Mungu kwa kupitia Fundisho la Kuhesabiwa Haki, ukweli ni kuwa watu hao hawaifahamu haki ya Mungu. Haki ya Mungu ni nini? Kwa kweli haki ya Mungu ni tofauti kabisa na haki ya mwanadamu. Haki ya Mungu inafunuliwa katika injili ipi? Inafunuliwa katika injili ya maji na Roho. Ikiwa tutaikataa injili ya maji na Roho pasipo kuiamini, basi hiyo ina maanisha kuwa tunasimama kinyume na Mungu. 
Hakuna anayeweza kukombolewa toka katika dhambi au kupokea haki ya Mungu bila kuiamini injili ya maji na Roho. Je, mtu anaweza kuwa kinyume na haki ya Mungu hata kidogo? Nimeamini na kuhubiri juu ya injili ya maji na Roho kwa muda mrefu lakini sijawahi kumwona mtu yeyote ambaye anaweza kusimama kinyume na injili hii. Hakuna hata mmoja anayeweza kusimama kinyume na injili ya maji na Roho kwa msingi wa Neno la Mungu kwa kuwa injili hii ya haki ya Mungu inatupatia ukombozi sahihi na mkamilifu kwa dhambi zetu. 
 

Ni Nani Anayeweza Kuwahukumu Wale Walio na Haki ya Mungu?
 
Hebu tusome Warumi 8:34. “Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Je, mtu yeyote anaweza kuwahukumia adhabu wale wanaoamini katika haki ya Mungu kuwa ni wenye dhambi? Hakuna hata mmoja anayeweza. 
Je, kuna mtu yeyote anayeweza kuwahukumia adhabu waamini wa injili ya maji na Roho ambao wamekombolewa toka katika dhambi zao kwa imani kuwa ni wenye dhambi? Hapana! “Ni nani atakayewahukumia adhabu?” Ni nani anayeweza kusema kuwa waamini wa haki ya Mungu ni wenye dhambi? 
Mshahara wa dhambi ni mauti. Ikiwa una dhambi katika moyo wako, basi utakwenda kuzimu. Mungu anawahukumu watu kwa kuwa wana dhambi. Lakini wale ambao dhambi zao zimechukuliwa mbali kwa imani yao katika haki ya Mungu hawawezi kuhukumiwa na Mungu, kwa sababu hawana dhambi ambayo wanapaswa kuhukumiwa kwa hiyo. Wakati Mungu mwenyewe hawahukumu wale wanaoamini katika haki ya Mungu, ni nani basi anayeweza kudiriki kuwahukumia adhabu? Ikiwa mwamini katika Yesu Kristo ana dhambi, basi mtu huyo ni mtenda dhambi na atahukumiwa adhabu ya Mungu. Wenye dhambi watahukumiwa na Mungu kwa sababu ya dhambi zao katika mioyo yao na pia watatengwa na watu wengine. Lakini ikiwa mwamini katika Kristo anaamini katika injili ya maji na Roho na anaipokea haki ya Mungu, basi mtu huyo hana dhambi mbele za Mungu na hakuna mtu anayeweza kumhukumia adhabu mtu huyo. Wala hakuna dhambi katika dhamiri za watu kama hao. 
“Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Yesu, Mwana wa Mungu, alikuja hapa duniani ili kutupatia haki ya Mungu, aliupokea ubatizo toka kwa Yohana Mbatizaji ili kuzibeba dhambi zetu zote, alikufa Msalabani na kuimwaga damu yake, na kisha akafufuka tena toka wafu ili kufanyika Mwokozi wetu. Sasa ameketi mkono wa kuume wa Mungu na anatuombea kama Mwokozi wetu. 
Pia Roho Mtakatifu anawaombea wale walio na haki ya Mungu. Yesu anatuombea huko Mbinguni. Pia Roho Mtakatifu anatuombea kwa Mungu Baba lakini kwa njia nyingine ya “kuugua” kusikoweza kutamkwa kila wakati tunapokuwa na udhaifu katika mioyo yetu. 
Kwa kweli haki ya Mungu ni kamilifu sana katika mioyo ya wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho. Ukamilifu wa haki ya Mungu unatueleza kuwa injili ya maji na Roho pia ni kamilifu na isiyo na mawaa.